Breaking News

BAWATA: Chanzo cha waganga matepeli ni mfumo



Na Komba Kakoa

BARAZA la Waganga wa Tiba Asili (BAWATA) limeiomba serikali kupitia Wizara ya Afya Kitengo cha tiba asili kuboresha mfumo wa usajili wa dawa  ili waweze kubaini matapeli wanaovamia taaluma hiyo huku wakijifanya wana uwezo wa kutibu.
Kwamba mfumo wa usajili ukiboreshwa wataweza kutengeneza umoja utakaosaidia kufanya kazi kwa umoja  na kuimarisha tiba asili hapa nchini na  hatimaye kusaidia wananchi wanaoteseka kwa maradhi.

Ombi hilo limetolewa na Mkurugezi wa Baraza hilo, Islam Makingili alipokuwa akizungumza na TABIBU kufahamu msimamo na kauli ya baraza hilo kuhusu tuhuma  ya utapeli dhidi ya baadhi ya waganga wa tiba asili.
“Tunachotaka hapa ni uboreshwaji wa mfumo wa usajili, kwani watu waliopewa jukumu la usajili hawana utaalamu wa tiba asili, hawana uwezo wa kuwatambua matatibu halisi na matapeli jambo ambalo kwa kiasi kikubwa linasababisha matapeli kutumia fedha zao kuvamia tiba yetu na kuwaumiza wananchi,” alisema.
Katikati ni Makamu mwenyekiti wa Bawata Mohamed Matokeo

Aliongeza kuwa wakati umefika sasa shughuli zote za usimamiaji wa tiba asili kwa kila ngazi kuhusisha waganga wenyewe wa tiba asili kwani wao wana mbinu mbalimbali za kuwabaini waganga halisi na matapeli kutikana na mfumo wa sasa kuruhusu kusajiliwa kwa watu wanaojiita waganga wakati hawajui lolote.
Pia alilalamikia waganga wa tiba asili kusumbuliwa pindi wanapohitaji kumuona mkemia mkuu wa serikali kwa ajili ya kufanya vipimo vya dawa zao, huku akilalamikia pia gharama kubwa za usajili wa dawa hizo.
Alidai kuwa awali gharama za kupima sampuli moja ya miti dawa ilikuwa Shilingi 300 000, lakini kwasasa  zimeongezeaka na  kufikia Sh. 750,000 kiwango ambacho sio rahisi kwa matabibu wenye mtaji mdogo kuweza kumudu na kusababisha wengi kuhudumia wagonjwa bila dawa zao kusajiliwa.
“Katika kila kijiji, mtaa, kata na wilaya kuna kamati za afya, lengo  likiwa ni kusimamia kupitisha fomu watu wanaoomba uganga, lakini jambo la kushangaza watu ambao hawana taaluma au uwezo wa tiba asili wanatumiwa kupitisha fomu za maombi ya waganga na kuwa chanzo cha kusajiliwa watu matapeli kwa kutumia fedha zao,”alisema.
Naye Mwenyekiti wa baraza hilo, Shaka Mohamed alilalamikia usajili wa dawa kwa njia ya dola kwamba na kusema kitendo hicho hakijengi uzalendo na kinaathiri ustawi wa tiba asili hapa nchini.
“Ni jambo la ajabu sana, kufanyika kwa miamala katika usajili huu kwa njia ya dola, huu ni uonevu, serikali iingilie kati suala hili ili Tanzania iende sambamba na mabadiliko ya tiba asili duniani, kwani baadhi ya nchi zimekuwa zikifanya usajili wa miti dawa bure na katika nchi hizo dawa za asili zimekuwa zikiyaingizia mataifa hayo fedha za kigeni,”alisema.
Pia aliishauri ofisi ya mkemia mkuu kutoa ufafanuzi wa matokeo ya vipimo vya dawa hizo kutokana na mfumo wa sasa huonyesha kiwango cha dawa au kemikali bila kufafanua madhara, matumizi na faida.

 “Waganga wanataka kiwango cha kemikali kilichomo, kiasi kinachooneshwa kwenye vipimo, kemikali hiyo iko chini au juu, nini faida au hasara na ushauri wa wa matumizi,  sio kuonyesha tu kiwango basi,”alisema.

Hakuna maoni