Breaking News

MUHAS yafafanua matumizi ya dola



Na KOMBA KAKOA
LICHA ya Serikali kupiga marufuku matumizi ya fedha za kigeni ikiwamo ‘dola’ lakini Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kimeendelea na utaratibu huo.

Kutokana na hali hiyo Chama cha Wataalamu wa Maabara Tanzania (MelSAT) kimeiomba Serikali ifuatilie suala hilo ambalo linadaiwa kusababisha mkanganyiko miongoni mwa wataalamu hao.
Akizungumza na Mtandao huu hivi karibuni ofisini kwake, Makamu wa Rais wa MelSAT, Peter Mwevila, alisema MUHAS imetangaza kozi ya kujiendeleza ya Usimamizi wa Maabara (Laboratory Management) kwa wataalamu wa maabara lakini malipo yameweka katika mfumo wa dola.
Hata hivyo alisema licha ya kozi hiyo kuwajumuisha watanzania lakini malipo yake yanatakiwa kulipwa kwa mfumo wa fedha za kigeni.
“Kama wataalamu wa maabara ambao ndio walengwa wakuu katika kozi hiyo lakini tunashangazwa na uongozi wa MUHAS kutaka wahitaji walipie mafunzo hayo kwa mfumo wa dola,”alisema Mwevila.
Kwa upande wake Mohamed Zuber ambaye ni mtaalamu wa maabara alisema kwamba ni kawaida kwa wataalamu wa fani mbalimbali kupatiwa mafunzo ama elimu ya kujiendeleza lakini si kwa gharama kubwa kama iliyoainishwa na MUHAS.
“Ili mtu afanye kazi kwa ufanisi ni lazima apewe mafunzo ya kujiendeleza na kupata maarifa mapya, lakini kama Mtanzania naona MUHAS hawajatutendea haki kuweka ada kwa malipo ya dola angalau wangetuwekea kiwango kidogo katika mfumo wa shilingi ili tujivunie chakwetu,”alisema Zuber
Kutokana na malalamiko hayo Mtandao huu ulimtafuta Afisa Uhusiano wa MUHAS, Hellen Mtui, ambaye alikiri kuwepo kwa kozi hiyo na kwamba inatarajiwa kuanza tarehe 12 Machi hadi 14 Aprili.
Alivyoulizwa kuhusiana na matumizi ya dola, Mtui alisema wanaolipa kwa mfumo wa dola ni wale wanaotoka sehemu mbalimbali lakini kwa watanzania wanalipa kwa shilingi.
Mtui alisema kwamba ni kozi fupi ya wiki tano kwa ajili ya wafanyakazi kujiendeleza (Continues development course) na inajumuisha watu kutoka sehemu mbalimbali.
“Kuhusiana na mfumo wa malipo ya fedha za kigeni ni kwa ajili ya wageni kwani kuna fomu nyingine ambazo zimeandaliwa kwa lugha ya Kiswahili kwa ajili ya Watanzania,”alisema Mtui.
Hata shivyo tangazo lililoshuhudiwa na Mtandano huu ambalo limetolewa kwa lugha ya Kingereza na MUHAS linaonyesha ada ya mafunzo hayo ni 1500 ambayo ikikokotolewa katika viwango vya Shilingi ni 3,375,000.
Ikumbukwe tu kwamba mwaka jana Rais John Magufuli alipiga marufuku matumizi ya fedha za kigeni huku Wazirin wa fedha Philip Mpango akibainisha kuwa Januari moja mwaka huu ilikuwa ndio mwisho wa kutumia fedha hizo katika huduma mbalimbali.
Aidha, Waziri Mpango alisema kwamba matumizi ya fedha za kigeni humuumiza mteja lakini pia huathiri uchumi wa nchi.
Aliongeza kuwa suala la matumizi ya fedha za kigeni limeendelea kuwa kero kwa wananchi kutokana na ugumu wa kusimamia matakwa ya sheria kwani baadhi ya wateja hupewa kiwango cha thamani  ya kubadilisha fedha ambacho kiko juu kuliko thamani halisi iliyoko kwenye soko.
Mwisho.

Hakuna maoni