Breaking News

Maisha magumu yadaiwa kuchochea ongezeko la wagonjwa wa akili





Na KOMBA KAKOA
WATAALAMU wanafafanua kuwa ugonjwa wa afya ya akili (Kichaa) ni tatizo kubwa linalowakumba watu wengi na kuathiri uwezo wa kufikiri, kudhibiti hisia na tabia jambo ambalo huvuruga uwezo wao katika kufurahia uhusiano mzuri na kukabiliana na changamoto za maisha.
Licha ya tatizo hili kuwa kubwa lakini linadaiwa kuongezeka kadri siku zinavyokwenda kutokana na kuhusishwa na imani potofu huku waathirika wakitelekezwa bila msaada wowote.
Ernest Mhusa ni Afisa Muuguzi katika fani ya Afya ya akili katika hospitali ya Lutindi iliyoko Korogwe mkoani Tanga, anasema kuwa ugonjwa huo una changamoto nyingi kutokana na ugumu wa maisha.
Dk. Mhusa anasema kuwa ugumu wa maisha humfanya mtu awe na msongo wa mawazo na kujiingiza katika ulevi wa kupindukia, matumizi ya dawa za kulevya, huku wengine wakirithi kutoka katika familia zao.
“Msongo wa mawazo husababisha matatizo ya Biochemistry kwenye ubongo ambayo hifanya homoni ya Dopmini kupanda kiwango cha juu na kumfanya mtu achanganyikiwe na kuzungumza mwenyewe huku akisikia kelele na sauti za watu wasioonekana,” anasema.
Anasema kuwa mambo mengine yanayosababisha matatizo hayo ni migogoro ya kifamilia, ndoa kuvunjika na matatizo mengine ambayo humfanya mtu kuwa na msongo wa mawazo ambao wakati mwingine husababisha homoni ya Dopmini kushuka na kuwa katika kiwango cha chini hivyo husababisha akate tamaa, kukosa amani na wakati mwingine atamani kujiua.
“Kwasasa vijana ndio wapo kwenye hatari kubwa kupata matatizo haya kutokana na matumizi ya vilevi kupindukia, dawa za kulevya aina ya Heroin, bangi, na kutafuna mirungi na nyingine jambo ambalo humfanya kuwa na hasira.”alisema.
Anaongeza kuwa kutafuna mirungi humfanya mtu akose usingizi jambo ambalo husababisha apate matatizo ya Biochemistry ambayo humsukuma kufurahia ama kusononeka wakati wote.
“Sababu nyingine ni kwamba kama mtu aliwahi kupata ajali anaweza kutibiwa akapona au akaugua malaria kali (Celebral Malaria) na akatibiwa na kupona lakini baada ya miaka kadhaa tatizo hilo linaweza kumpata,” anasema Dk. Mhusa.
Anaongeza kuwa, kwa mtu ambaye aliwahi kupatwa na shida ya uti wa mgongo na kutibiwa akapona pia yuko hatarini kupata shida hiyo.
Kwa upande wa Shirika la Afya Duniani (WHO) lilitoa taarifa kuwa magonjwa ya afya ya akili yanasababishwa na kushuka moyo, ugonjwa wa Schizophrenia na kubadilika-badilika kwa hisia na kueleza kuwa yanayowadhoofisha watu wengi ingawa huyapuuza huku wagonjwa wakiendelea kuaibika.

Kadhalika ripoti moja ya Shirika la Kitaifa la Magonjwa ya Akili nchini Marekani inasema kwamba ingawa magonjwa ya akili yana tiba, lakini nchini humo, takribani asilimia 60 ya watu wazima na karibia asilimia 50 ya watoto wenye umri wa kati ya miaka 8 hadi 15 wanaougua magonjwa ya akili hawakutibiwa katika mwaka uliopita.

TIBA YA UGONJWA WA AKILI
Katika kushughulikia matatizo ya afya ya akili mgonjwa anapaswa kufuata matibabu yaliyopendekezwa na madaktari wa magonjwa ya akili ikiwamo kufata ratiba maalumu atakayopewa na madaktari hao inayoeleza ni muda gani mgonjwa anatakiwa kufanya mazoezi, kulala usingizi wa kutosha na wakati wa kupumzika kila siku.
Pia kula lishe kamili, kuacha kutumia vilevi kupita kiasi, mgonjwa anapaswa hushirikiana na watu anaowaamini na wanaomjali.
============== 

Hakuna maoni