Breaking News

Bil 18 zatumika utekelezaji miradi ya maendeleo Ilala


ZAIDI ya sh. Bil 18 zimetumika katika utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika Halmashauri ya Manispaa ya Ilala katika kipindi cha miezi sita kuanzia Julai hadi Desemba mwaka 2017
Hayo yalibainishwa jana na Afisa Uhusiano wa Halmashauri hiyo,Tabu Shaibu, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Afisa Uhusiano-Halmashauri ya Manispaa ya Ilala, Tatu Shaibu akizungumza na vyombo vya habari jana

Shaibu alisema katika fedha hizo zilizotumika shilingi 8,844,643,432.62 ni mkopo kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya uboreshaji wa barabara zitakazosaidia kupunguza msongamano wa magari katika barabara za katikati ya mji.
“Barabara zilizoboreshwa kupitia mradi wa DMDP ni ya Olimpio yenye urefu wa Km 0.68 na hatua ya utekelezaji iliyofikiwa ni asilimia 96.10, Kiungani Km 0.68 asilimia 85.91, Mbaruku Km 0.38 asilimia 82.58, Kongo Km 0.28 hatua iliyofikiwa ni asilimia 89.84, Omari-Londo Km 0.53 hatua iliyofikiwa ni asilimia 84 pamoja na barabara ya Ndanda Km 0.35 hatua iliyofikiwa ni asilimia 86.
Pia Halmashauri imelipa fidia kiasi cha shilingi 3,109,872,121.52 kwa waathirika wa maeneo ambayo yanapitiwa na mradi huo ili kufanikisha utekelezaji wake.
Aidha, Shaibu alisema katika kipindi hicho Halmashauri imepeleka jumla ya Shilingi 8,524,000,000 kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo na kiasi kilichotumika ni shilingi 5,863,659,471
Alisema Halmashauri hiyo imejenga shule mpya nne kutokana na ongezeko la wanafunzi ambalo limetokana na mpango wa Serikali wa Elimu bila malipo.
“Shule za Msingi zilizojengwa ni Kidugala iliyopo Kata ya Chanika, Zavala Kata ya Buyuni, Uamuzi Kata ya Majohe na Kinyamwezi iliyopo Kata ya Pugu,”alisema Shaibu.
Pia vyumba vya madarasa 28 vilijengwa katika shule za Msingi Bonyokwa, Mongo la ndege Mbondole, Mji mpya, Kibaga, Bangulo na Misitu na madarasa sita kukarabatiwa likiwamo moja katika shule Kinyerezi na vyumba vitano katika shule ya Msingi Mchikichini.
Pia alisema jumla ya matundu ya vyoo yaliyojengwa katika shule hizo ni 96 na 40 yamejengwa katika shule za zamani ambazo ni Buyuni, Bwawani, Tungini na Kilimani.
Kwa upande wa Sekondari vyumba 37 vilijengwa katika shule za Ilala, Halisi, Nguvu mpya, Kerezange, Misitu, Viwege, juhudi, Abbuy Jumaa, Kisungu, Gerezani, Ugombolwa na Kasulu.
“Halmashauri imejenga vyumba vya madarasa viwili katika shule ya Sekondari Ilala, Halisi viwili, Nguvu mpya viwili,  Kerezange viwili, Misitu viwili, Viwege viwili, Juhudi 10, Abbuy Jumaa viwili, Kisungu viwili, Gerezani vine, Ugombolwa vitatu na Kasulu ambayo ni mpya vyumba vine,”alisema Shaibu.
Aidha Halmashauri hiyo imejenga matundu 91 ya vyoo ambayo ni 27 katika shule ya Halisi, Misitu nane, Juhudi 27, Abbuy Jumaa 15, Ugombolwa sita na 27 kwa shule ya Kasulu.
Aliongeza kuwa pia walifanikiwa kukarabati nyumba ya mwalimu katika shule ya Sekondari Kimanga sambamba na ununuzi wa samani.
Kadhalika aliongeza kwamba Halmashauri hiyo imechukua hatua ya ujenzi wa mabweni ya wanafunzi katika shule ya sekondari Mbondole iliyoko kata ya Msongola kwa lengo la kukabiliana na changamoto ya usafiri kwa wanafunzi wanaokaa mbali pamoja na ukarabati wa shule kongwe za jangwani, Azania na Pugu ambao unaendelea.
Kadhalika alisema wamekamilisha ujenzi wa mradi mkubwa wa Hospitali ya Mama na mtoto Chanika hivyo kupunguza vifo vya Mama na mtoto pia kupitia ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam jingo la Mama na Mtoto limejengwa katika Hospitali ya Amana likiwa na vitanda 100, na kufanya idadi ya vitanda kufikia 353 kutoka 253 hospitalini hapo.
Aliongeza kuwa Halmashauri hiyo imefanya ukarabati wa Majengo ya huduma za Mama na Mtoto katika Zahanati ya Msongola na Mvuti kwa kutumia mapatio ya ndani huku ikiendelea kutekeleza ukarabati wa jingo la mapokezi katika hospitali ya Amana, kukamilisha ujenzi wa zahanati ya Mbondole, ujenzi wa magonjwa ya mlipuko katika zahanati ya Kipawa, kukamilisha ujenzi wa Zahanati ya Lubakaya, kumalizia ujenzi wa Zahanati ya Bangulo
Shaibu alisema katika sekta ya maji halmashauri hiyo imeshaanza hatua utekelezaji katika miradi ya maji ikiwa ni pamoja na ukamilishaji na ukarabati wa miradi ya maji katika kata ya Minazi, Tabata, Majohe, Vingunguti, Sekondari Pugu, Mkera na Pugu Station.
“Ujenzi wa kisima cha maji Mtaa wa Mkera Kata ya Msongola, ujenzi wa tenki la la ujazo wa kuhifadhia maji kiasi cha lita 250,000 katika eneo la Pugu Kimani, ujenzi wa tanki la maji lenye ujazo wa lita 150,000 la kuhifadia maji katika Kata ya Kisukuru pamoja na miundombinu ya usambazaji maji katika eneo la Kata ya Mzinga,”alisema Shaibu.
Pia ujenzi wa Mradi wa maji Sharifu Shamba kata ya Ilala na Kata ya Kitunda, Kusambaza mabomba ya maji katika eneo la 511KJ Gongo la Mboto Jeshini.
Aidha Shaibu aliongeza kwamba katika kipindi hicho Halmashauri hiyo imepeleka Sh. 543,400,000 kwa ajili ya mikopo kwa wanawake, vijana na walemavu.
MWISHO

Hakuna maoni