Breaking News

Yaliyomkuta mkandarasi wa Uwanja wa Taifa Dar


Na Mwandishi wetu

*Alijenga chini ya kiwango, akanyongwa na Serikali ya China?


UWANJA wa Taifa uliopo jijini Dar es Salaam ni moja kati ya viwanja bora kabisa vya michezo barani Afrika, ukiwekwa nafasi ya pili kwa uzuri na gharama nyuma ya ule wa Soccer City uliopo Afrika Kusini.

Kwa Afrika Mashariki, uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watu 60,000 waliokaa unashika nambari moja ukivipiku viwanja maarufu kama Kasarani cha Kenya na Namboole Nelson Mandela kilichopo Mukono nje kidogo ya jiji la Kampala, Uganda.
Balozi wa China nchini, Dk. LU Youqing
Mara baada ya kumalizika kujengwa kwa uwanja huo na kukabidhiwa serikalini mwaka 2008, kumekuwapo tetesi kwamba mkandarasi aliyesimamia ujenzi huo aliujenga chini ya kiwango na hivyo kuikasirisha Serikali ya China iliyotoa fedha nyingi katika mradi huo.
“Wachina hawana mchezo na fedha zao, huyu aliyejenga uwanja huu aliporudi kwao akashitakiwa na kunyongwa. Sisi tunaona bonge la uwanja kumbe haujakidhi vigezo,” alisikika akisema shabiki mmoja wa soka ndani ya uwanja huo hivi karibununi.
Raia Tanzania lilifanya juhudi za kuufahamu ukweli wa suala hilo ambalo limeingia sana vichwani mwa Watanzania kujua sababu hasa za kunyongwa au kuadhibiwa kifo kwa mhandisi huyo.
Akizungumza jijini Dar es Salaam wiki iliyopita, mmoja wa maofisa wa Kampuni ya Beijing Construction Engineering Group ya China, alikanusha kuadhibiwa au hata kukamatwa kwa msimamozi yeyote wa mradi wa ujenzi wa Uwanja wa Taifa.
“Ni uvumi tu wa mitaani. Uwanja huu ulisimamiwa na wahandisi watatu na walipomaliza, walirejea China,” alisema ofisa huyo akiomba kutoandikwa gazetini kutokana na taratibu za kampuni hiyo, huku akishauri pia majina ya wahandisi hao yasiandikwe hadi baada ya kupata kibali kutoka makao makuu ya kampuni.
Kampuni hiyo inamilikiwa na Serikali ya Mji wa Beijing, ikijihusisha na ujenzi wa barabara, majumba makubwa, kufunga vifaa mbalimbali, usafirishaji, ujenzi na usanifu wa majengo.
Beijing Construction Engineering Group ni kundi la kampuni zipatazo 190 zikitoa ajira kwa zaidi ya watu 20,000 maeneo mbalimbali duniani.
Raia Tanzania liliambiwa na ofisa mmoja wa Ubalozi wa China nchini kuwa wasimamizi hao waliporejea nyumbani walitunukiwa tuzo mbalimbali na mmoja kati yao kwa sasa amechukuliwa na kuajiriwa serikalini.
Kwa ujumla, kampuni hiyo alipewa tuzo ya juu unayotolewa kila mwaka kwa kampuni iliyofanya vyema inayofahamika nchini China kama RUBAN kutokana na mradi huo.
“Ndio maana ninasema hakuna ukweli wa mtu kuhukumiwa sababu ya kuboronga ujenzi wa Uwanja wa Taifa. Uwanja ulijengwa kwa viwango vilivyotakiwa.
“Miongoni mwa kazi bora zilizowahi kufanywa na kampuni hii ni mradi wa Uwanja wa Taifa na baada ya kumalizika, tulipata kazi katika miradi mingine mikubwa ya kitaifa na kimataifa. Mengineyo ni upotoshaji mtupu,” alisema ofisa huyo wa ubalozi.
Taarifa zaidi zinadai kuwa China hakuna sheria ya kunyonga watu kwa makosa ya mradi kutekelezwa kwa kiwango cha chini.
Ofisa wa Beijing Construction Engineering Group aliyezungumza na gazeti hili jijini Dar es Salaam alisema katika utekelezaji wa mradi huo, mbali na ajira kwa Watanzania, kampuni pia ilichinba visima kama msaada kwa jamii inayozunguka eneo la mradi, ilijenga barabara na kuwafundisha Watanzania wengi usanifu na ujenzi.
“Mradi ulipokamilika, wengi walipata ajira kwenye kampuni nyingine kutokana na ujuzi tuliowapa. Hii yote ni michango yetu kwa Watanzania,” alisema.
Kama ishara ya kukubalika kwa kazi waliyoifanya, kampuni hiyo ilipewa miradi mingine kadhaa nchini baada ya Uwanja wa Taifa ikiwemo ujenzi wa Chuo Kikuu cha Sheria kilichopo Lshoto, Chuo Kikuu cha Dodoma, majengo ya Benki Kuu mjini Dodoma na sasa wanajenga Uwanja wa Ndege wa Mwanza.
Ujenzi wa Uwanja wa Taifa ulianza mwaka 2004 na Rais wa China, Hu Jintao akakabidhi ufungua wake kwa Rais Jakaya Kikwete mwaka 2008 baada ya ujenzi kukamilika.
Gharama za mradi huu ilikuwa Dola 60,000,000 ukitekelezwa na wataalamu 1,000 kutoka China huku ukitoa ajira kwa Watanzania 5000.
“Wakati mradi ukikabidhiwa kwa Tanzania mwaka 2008, Serikari ya Tanzania ilisema kwa wakati huu haina wataalamu na vifaa vya kukarabati uwanja huo ukiharibiwa au vifaa kuharibika wakati wa matumizi ya kawaida.

“Kwa hiyo wataalamu wa Kichina wa kampuni iliyoujenga waliendelea kuhudumia Uwanja wa Taifa, gharama zote za kitaalamu na ufundi zililipwa na Serikali ya China hadi Julai 2013 pale Balozi, Dk. Lu Youqing aliposaini mkataba na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Michezo kuukabidhi rasmi kwa serikali,” alisema. 
Chanzo:Raia Tanzania

Hakuna maoni