Breaking News

Walimu wanolewa kuhusu KKK, Na Mwandishi wetu, Bukoba


Walimu wa shule za msingi wamehimizwa kujenga na kuimarisha stadi za kusoma, kuandika na kuhesabu (KKK) kuongeza umahiri wa wanafunzi na mabadiliko chanya.
Hayo yalisisitizwa mwishoni mwa wiki na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Maendeleo ya Uongozi wa Elimu (ADEM) Bagamoyo, Dk. Siston Mgula, wakati wa ufunguzi wa mafunzo kwa walimu wa darasa la tatu na nne kutoka wilaya za Kyerwa na Missenyi mkoani Kagera.
 Walimu hao wanahudhuria mafunzo ya siku tisa ya mtaala mpya (ulioboreshwa) wa stadi za KKK katika Chuo cha Ufundi, VETA, mjini Bukoba.
 Dk. Mgula aliwataka walimu hao kuwaimarisha wanafunzi ili stadi hizo ziweze kuwajenga katika kujitegemea na kuleta mabadiliko chanya kwao na kwa taifa.
 Akimkaribisha Dk. Mgula, mratibu wa mafunzo hayo, Bernard Merumba, alisema walimu 388 wapo tayari kwa mafunzo hayo.
 “Hii ni awamu ya mwisho ya mafunzo kwa walimu wa Mkoa wa Kagera na tayari walimu 1,770 tayari wamepata mafunzo,” alisema.
 Hadi mwisho wa programu hiyo, walimu 23,000 nchini watakuwa wamehudhuria mafunzo hayo na kutunukiwa vyeti.
 Mwenyekiti wa mafunzo, Mwalimu Anatoria Joram wa Shule ya Msingi Ishunju wilayani Missenyi, alimuahidi Dk. Mgula ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye mafunzo hayo kuwa watayatumia maarifa waliyopata kwa manufaa ya taifa na kuyapeleka pia kwa wenzao ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.


Hakuna maoni