Breaking News

Waliochoma moto shule kukiona-Na Mwandishi wetu - MAELEZO


 SERIKALI imesema itawachukulia hatua kale wote watakaobainika kwa sababu moja au nyingine kuhusika na matukio ya moto yaliyotokea mkoani Arusha hivi karibuni.
Hayo yalisemwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu Sayansi na Teknolojia, Profesa Simon Msanjila katika mahafali ya tano ya Shule ya Msingi ya Macedonia iliyopo Tabata Segerea jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki.

Akizungumza kwa niaba ya Profesa Msanjila, Mkurugenzi wa Elimu ya Msingi wa wizara hiyo, Sarah Mlaki, alilaani matukio hayo.
Alisema mbali na kuwachukulia hatua wahusika, Serikali imechukua hatua mbalimbali kudhibiti majanga ya moto katika shule za sekondari za bweni nchini.
Jengo la shule ya sekondari Njombe likiwaka moto baada ya kuchomwa na wanafunzi

“Tutachukua hatua stahiki kwa wale ambao watabainika kwa sababu moja au nyingine wanahusika na majanga hayo,” alisema Mkurugenzi Mlaki.
Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa Serikali pia imejipanga kuboresha miundombinu ya shule zake ili watoto Watanzania wapate haki yao ya msingi ya kupata elimu.
Kwa upande mwingine, Mlaki alisema soko la vitabu vya kiada vinavyotumika katika shule za msingi nchini limevamiwa na watu mbalimbali na Serikali inafahamu kuwa kuna vitabu vingine havina ubora unaostahili kwa matumizi ya shule.
Alisema Serikali kupitia Taasisi ya Elimu Tanzania (TEA) imepewa dhamana ya kuandaa vitabu vya kiada ili wanafunzi wote kutumie vitabu hivyo bila ya kuwa na tofauti katika elimu inayotolewa.
“Ninaamini tatizo hilo litatatuliwa kadri siku zinavyokwenda kwa kuwa taasisi husika tayari inalishughulikia kulingana na uzito wake,” alisema.
Katika mahafali hayo, jumla ya wanafunzi 53 wa shule hiyo walihitimu na wanatarajia kufanya mitihani ya taifa ya darasa la saba mwaka huu, wakiwemo 24 wanaume na wanawake 29.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Shukuru Mbwire alisema shule hiyo iliyoanzishwa mwaka 2009, imekuwa ikifanya vizuri katika mitihani ya darasa la saba na la nne ambapo ilianza na wanafunzi 70 lakini hadi sasa ina wafanuzi 782.

Alisema katika matokeo ya mitihani ya kitaifa ya darasa la saba shule hiyo imekuwa ikifanya vizuri mwaka hadi mwaka ambapo katika mitihani ya mwaka 2015 shule hiyo ilipata wastani wa daraja A na kushika nafasi ya 3 kati ya shule 56 kiwilaya, nafasi ya 28 kati ya shule 534 kimkoa na kitaifa ilishika nafasi ya 219 kati ya shule 16,096.

Hakuna maoni