Breaking News

Mvua zijazo na majanga yake





Na Mwandishi wetu

MAMLAKA ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imetoa taarifa ya kuwapo mvua kidogo zitakazonyesha kwa kiwango chini ya wastani, ambayo kitaalam zinaitwa ‘La Nina.’

Mvua hizo katika lugha ya kawaida na hawa kwa wakulima zimezoeleka kama ‘Mvua za Vuli’ au ‘za kupandia’ na zinatarajiwa kunyesha kuanzia mwezi ujao, Novemba na Desemba.
 
Kulia Mkurugenzi wa Mamlaka ya Hali ya hewa Tanzania (TMA) Joyce Kijazi akiwa na Mkurugenzi wa Utabiri Hamza Kabelwa.
Dk. Agnes Kijazi, anasema kitaalam mvua hizo zimepewa majina tofauti kama vile ‘El Nino’ kwa mvua kubwa. Mvua hizo ziliwahi kunyesha nchini mwaka 1990.   
 “Unajua wataalam walitupa jila la ‘El- Nino’ wakati zilinyesha mvua nyingi, lakini kwa sasa wamesema tena kunapotokea mvua za chini ya wastani katika msimu wa mvua wanasema zinaitwa ‘La Nina,” anasema Dk. Kijazi.
 Mkurugenzi huyo anasema, wakati sehemu nyingi za nchi zinatrajiwa zisipate mvua kwa kiwango kinachotarajiwa, isipokuwa maeneo ya pembezoni mwa Ziwa Victoria na Kusini mwa nchi.
 Dk. Kijazi anasema katika kipindi hicho cha miezi mitatu aliyoitaja, matarajio ni mvua kuanza mwezi ujao katika ukanda wa Ziwa Victoria na baadhi ya maeneo ya mikoa ya Pwani na Kaskazini mwa nchi.

KWA NINI MVUA?
Dk. Kijazi anasema hali hiyo ya joto, inaashiria kuwapo upepo wenye unyevunyevu hafifu kutoka Mashariki, kuelekea Pwani ya Afrika Mashariki.
Pia, anasema kuongezeka joto la baharini, jirani na pwani nchi ya Angola, hususan katika miezi hiyo mitatu, inachangia kuwapo upepo wenye unyevu kuanzia ukanda wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), hadi Kusini-Magharibi ya Tanzania.

Dk.Kijazi anasema hali hiyo inaelezwa kusaidia kupunguza matukio ya vimbunga nchini.

HALI YA BAADAYE
Dk. Kijazi anasema, bado hali ya mvua si kitaifa salama sana. Maeneo mengi yanatabiriwa kuwa na upungufu wa mvua katika siku zijazo.
Kutokana na hilo, mkurugenzi huyo wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), anasema kuna uwezekano wa kutokea athari katika sekta mbalimbali, pamoja na kuathiri utekelezaji wa majukumu zake.

Anataja sekta husika kuwa za Kilimo na Usalama wa Chakula, Nishati, Afya, Maji na ofisi zinazohusika na Mamlaka za Miji na Menejimenti ya Maafa.
Hali ngumu ya upatikanaji mvua inatarajiwa kuleta ugumu katika ustawi wa mazao ya kilimo katika maeneo mengi nchini, kutokana na mtiririko mdogo wa maji.
Dk. Kijazi anaongeza kuwa, vina vya mito na mabwawa nchini vinatarajiwa kupungua kutoka katika hali yake ya kawaida ambayo imezoeleka.
Anasema ni mazingira yanayoendana na  hatari ya kutokea mlipuko wa magonjwa katika baadhi ya maeneo nchini, chanzo kikuu kikiwa ni uhaba wa maji safi na salama.

USHAURI KWA WAKULIMA
Dk. Kijazi anasema mvua za kutoridhisha katika miezi, kunahatarisha mazao na malisho ya mifugo.
Ushauri wake kwa wakulima ni kwamba, waandae mashamba na pembejeo mapema na kwa kuzingatia ushauri wa maofisa ugani wa kilimo, kuhusu matumizi sahihi ya ardhi na mbegu.

Jingine wanaloshauriwa wakulima ni kutumia kwa uangalifu akiba ya chakula na kuangalia namna ya kulima mazao yanayohimili hali ya hewa ya kipindi hicho.
Matumizi hayo yanahusu kuzingatia
kilimo cha umwagiliaji na kuzalisha mazao ya chakula ya muda mfupi.
Katika maeneo yanayokabiliwa na upungufu wa malisho na maji ya mifugo na wanyama pori, Dk. Kijazi anawashauri wakulima wa maeneo hayo kuhifadhi chakula kwa ajili ya malisho ya mifugo.
Ubashiri wa Dk. Kijazi kuhusiana na athari ni uhaba wa mvua utaosasabisha uhaba wa malisho, utaibua migogoro baina ya wakulima na wafugaji, katika maeneo wanayoishi jirani.

Anatoa ufafanuzi kwamba, ni jambo linaloweza kuharibu mimea ya kilimo na kuleta ukosefu wa chakula cha kutosheleza.
Katika hilo, Dk. Kijazi anashauri mamlaka zinazosimamia wanyamapori na jamii, iishio katika maeneo hayo kuchukua hatua stahiki dhidi ya migogoro inayoweza kujitokeza katika maeneo mengi ambayo huenda yakakumbwa na mvua.
Anasema mamlaka zinazosimamia huduma za utalii na uhifadhi za wanyamapori zinapaswa kuchukua hatua madhubuti, ikiwamo kuzuia uharibifu wa miundombinu hususan barabara na madaraja, yaliyomo ndani ya hifadhi.

MAMLAKA ZA MIJI

Dk. Kijazi ambaye ametoa tahadhari katika maeneo mengi kulingana na usalama wa hali ya hewa, anawasihi wananchi
wahakikishe wanaweka mifumo bora wa njia za kupitisha maji katika kipindi cha mvua.
Anasema kuna uwezekano wa kuwapo mvua nyingi ndani ya kipindi kifupi, hivyo ni muhimu kutolewa tahadhari kutoka kila upande wa nchi kuhusiana na mwenendo huo wa mvua.
Kwa mujibu wa Dk. Kijazi ni kwamba, hata katika baadhi ya maeneo ambako kunakadiruwa kuwapo mvua za kipindi kifupi, kunaweza kuwapo mvua nyingi katika kipindi kifupi.

Anasema kutokana na uhaba wa maji safi na salama ambayo ina atahri kubwa katika shughuli za kibinadamu katika kipindi hicho, wananchi wanashauriwa kuchukua hatua za kujihadhari kupitia matendo yao.
Dk. Kijazi anaikumbusha Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kuchukua tahadhari ya kuchukua hatua zinazotakiwa kuepusha athari zinazoweza kujitokeza.
Mkurugenzi wa TMA anatoa rai kwa wanahabari na vyombo vyao kusaidia kutoa taarifa sahihi kwa wananchi, kuhusu  mwenendo wa mvua katika kipindi hicho chote.
Pia anawaomba wananchi kujenga tabia ya kufuatilia kwa makini taarifa zinazohusu hali ya hewa, ili kujihadhari kwa kadri inavyopaswa.

@Nipashe

Hakuna maoni