Elimu haiwezi kupiga hatua masilahi ya walimu yasipozingatiwa
Na
Komba Kakoa
RIPOTI
ya taasisi ya Twaweza ya tathimini ya elimu kwa watoto ya mwaka 2014 imebaini udhaifu
mkubwa wa wanafunzi wa darasa la saba
jambo ambalo ni dhahiri kuwa hali hiyo inatishia maendeleo ya elimu hapa
nchini.
Kupitia
mradi wake wa uwezo, Twaweza wanasema kuwa wanafunzi wanne kati ya kumi wa
darasa la saba sawa na asilimia 44 hawawezi kusoma hadithi kwa lugha ya Kiingereza
ya kiwango cha darasa la pili.
Wawili
kati ya 10 ambayo ni sawa na asilimia 16
kadhalika hawawezi kusoma hadithi ya Kiswahili ya kiwango cha darasa la pili.
Pia wawili kati ya 10 sawa na asilimia 23 hawawezi kufanya hesabu za kuzidisha
za kiwango cha darasa la pili.
wanafunzi wa darasa la kwanza wakiwa darasani |
Meneja
wa mradi huo, Zaida Mgalla anasema kuwa watoto 32,694 walipimwa katika masomo hayo kutoka kaya 16,013 za wilaya 50
za Tanzania Bara katika jumla ya shule za msingi 1,309 za nchini humo.
“Tulilenga
kuwapima watoto wenye umri kati ya miaka saba hadi 16 kupitia wakusanya takwimu
wa kujitolea 2,626 ambao walikuwa wakitathmini watoto hawa...katika utafiti
wetu tulibaini kwamba watoto kutoka familia zenye uwezo hasa mjini wana uwezo
mkubwa zaidi wa kupata stadi za msingi za kusoma na kufanya hesabu kuliko
wenzao wanaotoka familia masikini au wanaoishi vijijini,”alisema.
Mgalla
anasema pamoja na mafanikio yanayoonekana kwenye ongezeko la uandikishaji wa
wanafunzi, Tanzania bado haijatimiza dhamira yake iliyojiwekea ya mpango wa ya elimu
bure kwa wote kutokana na kukosekana kwa usawa kwenye vifaa vya shule, mazingira
mazuri ya kujisomea, uandikishaji na matokeo ya kujifunza.
Anasema
juhudi za kuhakikisha kuwa watoto wanaelewa vizuri wawapo darasani sio tu
katika kununua madawati au ujenzi wa madarasa bali ni uwekezaji katika idara ya
walimu kwa kulipwa madai yao yote pamoja na kuboreshewa mazingira yao ya kazi.
Mkurugenzi
Mtendaji wa Twaweza, Aidan Eyakuze anasema kuwa kamwe elimu haitaweza kupiga
hatua iwapo masilahi ya walimu yasipozingatiwa.
“Popote
pale uendapo, kama waalimu hauwathamini
hakuna kusoma, hivyo wadau wana wajibu wa kushirikiana na serikali ili kuwaboreshea
mazingira mazuri walimu hao,”anasema.
Katika
ripoti hiyo, imeelezwa kuwa matokeo ya masomo yote matatu yaliyopimwa na
tathmini ya uwezo ya mwaka huo yameendelea kuwa chini.
Katika
ripoti hiyo asilimia 54 ya wanafunzi wa darasa la tatu ndiyo wanaoweza kusoma hadithi
ya Kiswahili ya darasa la pili. Kuhusu hadithi ya Kiingereza asilimia 19 ya wanafunzi wa darsa hilo ndiyo wanaoweza kusoma
hadithi kwa lugha hiyo kwa kiwango cha darasa
la pili na asilimia 35 pekee wanaweza kufanya hesabu za darasa la pili.
Mgalla
anasema katika kipindi cha miaka mitano ya tathmini ya mradi huo, kumekuwa na
mabadiliko finyu kwenye matokeo ya kujifunza na kusema kuwa viwango vya ufaulu
wa somo la Kiswahili vinaonyesha matokeo chanya.
“
Kwa mfano mwaka 2012 na 2014, idadi ya wanafunzi wa darasa la tatu ambao
wanaweza kusoma hadithi ya Kiswahili ya darasa la pili imeongezeka kutoka asilimia
26 hadi 54,” anasema
Kuhusu
tatizo la utoro anasema nusu ya asilimia 19.2 ya watoto ambao hawakuwa shuleni
walionaika kwenye utafiti huo wanatoka kwenye kaya masikini.
Pia
anasema kuna utofauti kubwa kati ya mkoa mmoja na mwingine katika idadi ya watoto
wenye umri wa miaka saba hadi 16 ambao hawapo shuleni ambapo asilimia 8 ya
watoto wanaotoka mkoani Dar es Salaam wenye umri wa miaka 7 hadi 16 hawapo
shuleni ikilinganishwa na asilimia 35 wa mkoa wa Shinyanga.
Kwa upande wa mazingira
ya shule, ripoti imebainisha kuwa utoro wa walimu umekuwa ni tatizo sugu ambalo
linalowaumiza watoto katika kujifunza.
Kwa
mwaka 2014, asilimia 31 ya walimu
hawakuwa shuleni wakati tathmini hiyo inapita ikilinganishwa na mwaka 2012
ambapo ilikuwa asilimia 21.
Aidha
kuhusu uwiano wa wanafunzi na walimu nao ni tofauti ; wanafunzi 126 kwa mwalimu
mmoja katika mkoa wa Mara na wanafunzi 56 kwa mwalimu mmoja katika mkoa wa
Pwani.
Kwa
upande wa vitabu, ripoti inaonyesha kuwa wanafunzi 26 kwa kitabu kimoja mkoani
Tabora na wanafunzi watatu kwa kitabu kimoja mkoani Mtwara, Kilimanjaro, Katavi,
Ruvuma na Njombe.
Kwa
upande wake, Meneaja Mkuu wa mradi huo wa Uwezo Afrika Mashariki, Profesa John
Mugo anasema kuwa matatizo ya kielimu kwa nchi za ukanda huo yanafanana ingawaje
kuna utofauti kidogo.
Anasema
kuwa kwa nchi ya Kenya, walimu ambao hawafiki darasani ni asilimia 11 tu
ikilinganishwa na Tanzania yenye kiwango cha asilimia 31 ya utoro wa walimu
kazini.
Mwalimu
Mkuu wa Shule ya msingi ya Nsongwanhala iliyopo Nzega , George Mgina, anasema
kuwa katika ripoti hiyo, changamoto nyingi zimeonekana huku kubwa zaidi likiwa
ni utoro wa waalimu jambo ambalo kwa namna moja au nyingine limesababisha wanafunzi
kushindwa kufanya vizuri licha ya kupewa masomo rahisi wakati wakiwa katika
ngazi za juu.
”Bila
ya Mwalimu hakuna shule, hakuna kusoma wala kujifunza, kwa hiyo suala hili
lisipoangaliwa kwa makini, elimu yetu bado itasalia kuwa shakani huku mataifa
jirani yakiendelea kutupita,”anasema.
Moja
ya wasomi mahiri na wachambuzi wa masuala ya elimu nchini, Profesa wa chuo
kikuu cha Dar es Salaam, Kitila Nkumbo, anaunga mkono hoja ya walimu kutopewa
stahiki zao kwa wakati jambo ambalo linasababisha kuwepo kwa matokeo hasi kwa
wanafunzi wengi.
Anasema
kuwa elimu si bahasha, bali ni uwezo wa mwanafunzi katika kuhakikisha
anapanukia kiuelewa na kifikra, kuwa na mawazo thabiti na yenye nguvu ambayo
yanayoweza kuwa kichocheo katika maendeleo.
“Kuweka
dawati zuri, vitabu vizuri haikidhi kuonyesha kuwa ndiyo umemaliza jitihada za
kuboresha elimu, daima mwalimu ndiyo nguzo katika kitivo hicho cha elimu, hivyo
anastahili kuangaliwa kwa umakini zaidii,”anasema.
Utafiti
huo ni wa tano sasa, kutoka mwaka 2010 hadi 2014 , lengo kuu likiwa ni kuangalia kiwango cha watoto katika
kuwapima kujifunza kinadharia na vitendo kwa ajili ya ustawi wa Taifa.
Ingawaje
Twaweza wamekuwa wakijitolea katika kufanya tafiti hizo, matunda yake bado yanaonekana
kulega kutiliwa mkazo na serikali hasa katika suala zima la mahitaji ya walimu
hivyo jitihada za ziada zinahitajika ili kulikomboa taifa letu dhidi ya adui
aitwaye ujinga kama ambavyo Mwalimu Julius Nyerere aliwahi kunukuliwa katika
moja ya hotuba zake enzi ya uhai wake.
“Tuna
maadui watatu, ujinga, umasikini na maradhi, tunapaswa kupambana nao ili
kuwashinda,”alinukuliwa Hayati Mwalimu Nyerere katika moja ya hotuba zake.
Hakuna maoni