Breaking News

Ziara ya Kinana 2014 na majipu ya Rais Magufuli



KATIKA moja ya ziara za mikoani za kuimarisha chama, Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana, aliwahi kuainisha upungufu katika utendaji wa serikali na kueleza kuwa umesababisha wananchi kukilalamikia chama hicho.
Akasema kuwa anatambua kuwa kuna upungufu na makosa ya kiutendaji ikiwamo kushamiri kwa rushwa na upendeleo serikalini jambo ambalo linasababisha wananchi kuilalamikia serikali na CCM.
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana akisalimiana a wananchi kwa bashasha, alipowasili katika kijiji cha Nyan'kanga, katika jimbo la Buanda mkoani Geita

Hii ilikuwa ni mwaka 2014 wakati akiitimisha ziara yake mkoani Singida kwa kufanya mkutano wa hadhara kwenye uwanja wa Peoples na kusema kuwa watendaji serikalini wamekuwa wakitumia ufumbuzi wa muda kama kuzima moto na akapendekeza kuwa lazima tujenge utaratibu wa kumaliza matatizo ya wananchi uwe wa mipango ya muda mrefu.
Kinana aliutaja upungufu mwingine kuwa ni uwajibishaji wa watendaji wabovu, wakati wanaharibu utawala bora haushiriki ila akishaharibu ndio utawala bora unaanza.
"Inaundwa tume ya uchunguzi, kisa utawala bora, sipingi utawala bora bali napinga unaolalia upande mmoja…dhambi kabla haijatendaka hatua hazichukuliwi ila ukishakamilika ndiyo unachukuliwa,” akasema Kinana.
Katibu huyo akakosoa utaratibu wa kuwahamisha watendaji wanaotuhumiwa kwa utendaji mbovu na wizi, huku ikielezwa kwamba hakuna ushahidi wa kuwatia hatiani.
Akasema kuwa ni lazima nidhami iongezeke serikalini, uwajibishaji, kuchukua hatua mapema na kwamba imekuwa kawaida kwa jambo dogo kuachwa muda mrefu ikiwa ni pamoja na watu kwenye kituo kingine kabla ya kuchukuliwa hatua.
Nimejaribu kueleza kwa kirefu kile ambacho Kinana aliwahi kukisema katika ziara zake kwa lengo la kuelezea kile ambacho sasa kinafanywa na Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Dk. John Magufuli.
Ikumbukwe kuwa mbali na hayo, Kinana aliwahi kuwaita baadhi ya watendaji wa serikali ya awamu ya nne kuwa ni mzigo akawa anashauri waondolewe kwenye nafasi zao.
Katibu huyo alikuwa akilalamikia udhaifu aliokuwa akiuona katika serikali hiyo na sasa umeanza kushughulikiwa na Rais Magufuli na timu yake ili kurudisha nchi kwenye mstari.
Ninaweza kusema kuwa alichokuwa akikifanya Kinana ni kumuonyesha rais wa sasa majipu na sasa anaendelea kuyatumbua kila anapoyabaini ili kuhakikisha hakuna malalamiko ndani ya jamii kama huo ulioelezwa na katibu huyo.
Hata Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi, (Bara), Philip Mangula, juzi aliweka wazi kuwa kila anachokifanya Rais kina mkono wa CCM na anaunga mkono utendaji kazi wa rais.
Waswahili wana msemo wao usemao kuwa ukiona mwenzio ananyolewa na wewe tia maji, hivyo wakati Rais Magugfuli akiendelea kutumbua majipu kwa watendaji wa umma, CCM nao wajiandae kutumbuliwa.
Kwa sababu anachokifanya kina mkono wa CCM kama alivyosema Mangula na pia hakuna siri kwamba ndani ya CCM kuna majipu ambayo nayo yanahitaji kutumbuliwa ili chama kirejeshe heshima yake mbele ya umma wa Watanzania.
Chama kuwa na majipu siyo kauli yangu bali ni ya Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan ambayo aliwahi kuitoa mkoani Tanga kwamba kuna watu majipu ndani ya CCM ambao wameficha makucha ili wasijulikane uovu wao.
Hilo Rais Magufuli mwenyewe analijua kwa sababu alishawahi kusema kwamba ndani ya chama hicho kuna watu wanafiki, ambao mchana wanakuwa CCM na ukifika usiku wanakwenda upande wa wapinzani.
Mwisho.

Hakuna maoni