Breaking News

Mechi Dar Kambi Uturuki, hii haiko sawa!!




Na Komba Kakoa


MABINGWA wa Tanzania,  timu ya Yanga ya jijini Dar es Salaam imeianza vibaya michuano ya kombe la shirikisho barani Afrika hatua ya makundi, baada ya kufungwa bao 1-0 na wenyeji wao Mo Bejaia ya nchini Algeria.
Ni dhahiri kwamba Yanga ilijiandaa kisayansi zaidi kuingia katika mchezo huo na matokeo hayo yametokana na kuzidina mbinu na waarabu hao ambao hawakuonyesha kiwango cha kutisha sana.
Lakini si kwamba Yanga walipoteza mchezo huo kutokana na ufinyu wa maandalizi bali tofauti tu za kimbinu ambazo kama wanamichezo tunafahamu kwamba mmpira wa miguu una matokeo ya aina tatu, yaani kushinda, kushindwa ama kutoka sare.
Lakini kwa kujua hali ya hewa ya Algeria kuwa ni baridi, Yanga waliamua kwenda kuweka kambi nchini Uturuki ambako kuna ya baridi pamoja na kuendelea na program za kufanya mazoezi usiku, muda uliolandana sawa na ule ambao mchezo ulipangwa kuchezwa, kweli haya ndio maandalizi ya kisayansi yaliyofanikishwa na kocha, wachezaji pamoja na benchi la ufundi.
Ni jambo zuri na lakuigwa kwa timu zetu za hapa nyumbani kuwa na maandalizi ya hali ya juu ambayo ni ya Kisayansi ili kuweza kuendana na hali halisi ya upinzani.
Kwamba timu nyingine za Tanzania zinapaswa kujifunza aina hii ya maandalizi ili kufikia mafanikio pia itakuwa kituko kwa timu inayojiandaa kwenda kucheza nchi za ukanda wa joto iweke kambi sehemu yenye baridi. Hii haiku sawa kabisa.
Yanga sasa inajiandaa na mchezo wa pili dhidi ya TP Mazembe unaotarajiwa kuchezwa Juni 28, katika dimba la Taifa jijini Dar es Salaam. Nilishtuka nilipopokea taarifa kuwa timu hiyo inaanza safari ya kurejea Uturuki katika mji wa Antalya kuendelea na kambi yake, nikajiuliza 'Yanga wamesahau nini tena Uturuki?'
Kocha yoyote anapenda mazingira tulivu ili aweze kuhakikisha mafundisho yake yanawaingia vizuri wachezaji, hii yaweza kuwa sababu kubwa iliyowafanya  Wababe hao wa mitaa ya Twiga na Jangwani wanogewe na kambi ya Antalya, lakini wamejiuliza kuhusu hali ya hewa?
Sidhani kama ni sahihi kwa Yanga kuendelea na kambi ya Antalya wakati wanajua hali ya hewa ya kule ni tofauti kabisa na ya Dar es Salaam, ambako mchezo unatarajia kuchezwa.
Ingekuwa vyema kama Yanga wangerejea nchini na kutafuta eneo ama mkoa ambao wanaamini kuna utulivu ikiwezekana kwenda hata visiwani ambako wamezoea kuweka kambi kujiwinda.
Licha ya mwezi mtukufu wa Ramadhan, Pemba panabaki kuwa sehemu tulivu na sahihi zaidi kwa Yanga kuelekea kuwavaa Mazembe ambao wenyewe wameanza vizuri michuano hiyo kwa kuifumua Medeama mabao 3-1 jijini Lubumbashi.
Acha nijifariji kuwa Yanga watapumzika  tu pale Antalya kwa siku moja kabla hawajaanza safari ya kurejea nchini, hawatoweka kambi kama ilivyoelezwa kwavile kufanya hivyo ni kujiongezea ugumu wa mechi.
Kutokana na uwepo wa mechi jijini Dar es Salaam, jiji ambalo lina hali ya joto, Yanga wamekosea kuweka kambi Uturuki ambako kuna hali inayotofautiana na eneo ambalo mchezo unatarajia kuchezwa.
====================== 

Hakuna maoni