Breaking News

UKATILI-Mwanafunzi asimulia alivyoteswa na walimu

NI ukatili. Hilo ndilo neno lililokuwa likitumika kuelezea mkasa uliohusisha kipigo alichokipata mwanafunzi wa kidato cha tatu katika Shule ya Sekondari Mbeya Day, Sebastian Chinguku.
Akizungumza na Nipashe kwa mara ya kwanza jijini humo jana, ikiwa ni baada ya kupata nafuu kufuatia tukio hilo lililozua mjadala mkali bada ya video yake kusambaa kwenye mitandao ya kijamii, mwanafunzi huyo, alisema amefarijika kutokana na hatua iliyochukuliwa na Serikali dhidi ya walimu waliomfanyia ukatili huo ambao kamwe hakuutarajia. Walimu hao walioonekana kwenye video iliyotikisa kwenye mitandao ya kijamii kuanzia juzi, wakimpiga Chinguku, ni Frank Msigwa na John Deo, amabo ni wanafunzi wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Elimu cha Dar es Salaam, (Duce) na Sanke Gwamka wa Chuo cha Ualimu cha Mwalimu Nyerere. Wote walikuwa katika mafunzo ya vitendo.
Mwanafunzi aliyefanyiwa Ukatili, Sebastian Chinguku

Hata hivyo, Chinguku alielezea kusitikishwa kwake na hatua iliyochukuliwa dhidi ya Mkuu wa Shule, Magreth Haule.
Akizungumza na Nipashe jana muda mfupi baada ya kutoka katika Hospitali ya Kanda ya Rufaa Mbeya, Chinguku alisema hatua ya Serikali ya kuwavua ualimu wahusika wa ukatili huo ni sahihi kwa sababu kipigo walichompa kilihatarisha maisha yake na siyo kwa nia ya kumfundisha kama ilivyo dhamira ya walimu wengine.
“Kwakweli walimu wale walionekana kama walikuwa na dhamira ya kuniua kutokana na kipigo… hawakuwa na utaratibu. Walikuwa wakinipiga popote pale kwa kutumia fimbo, mateke, ngumi na makofi huku wakiniburuza chini,” alisema na kuongeza:
“Wakati wakifanya hivyo, walisistiza kuwa wao wamepitia JKT (Jeshi la Kujenga Taifa) na hivyo siwezi kuwababisha… nashukuru niko hai. Naishukuru pia Serikali kwa hatua ilizochukua.”
Akieleza kuhusu adhabu aliyopewa mkuu wa shule ambaye amevuliwa madaraka, Chinguku alisema hana mamlaka ya kuzuia, lakini anaamini kuwa hastahili kaudhibiwa kwa tukio hilo kwa sababu upo uwezekano kuwa baadhi ya walimu walimficha kilichotokea kwa sababu hakuwapo na ndiyo maana hakuchukua hatua.
 
Waziri wa Elimu, Joyce Ndalichako
CHANZO CHA KIPIGO 
Akisimulia chanzo cha kufanyiwa ukatili huo, alisema kuwa ni kisasi walichokuwa nacho walimu hao dhidi yake kutokana na hisia kwamba yeye ni mjeuri, hasa kutokana na ukweli kuwa tayari alishakorofishana na mmoja wao kabla ya siku ya tukio.
Akisimulia zaidi, Chingukwa alisema kuwa siku ya Ijumaa, Mwalimu Msigwa alitoa zoezi lakini yeye hakuwapo shuleni siku hiyo na hivyo akashindwa kufanya kazi iliyotolewa naye (Mwalimu Msigwa).
Alisema baada ya hapo, ilipofika Jumatatu, mwalimu huyo (Msigwa) alifika darasani na kuamuru wale wote ambao hawakufanya kazi aliyotoa wapite mbele. Akawatandika wote fimbo tatu kila mmoja.
Alisema ilipofika zamu yake ya kuadhibiwa, yeye alijaribu kujitetea kuwa hakuwapo siku hiyo ya kutolewa kwa kazi hiyo.
Alisema jibu hilo halikumridhisha mwalimu ambaye alimshika na kwenda naye ofisini ambako walimu wengine waliokuwa kwenye mazoezi ya vitendo walikuwamo na kuanza kumpiga hovyo kwa fimbo, ngumi na mateke.
Alidai kuwa awali, mmoja wa walimu hao aliwahi kukorofishana naye kutokana na kuamuriwa avue sweta siku ya mtihani lakini yeye akakataa kwa kujitetea kuwa anaumwa na ndipo naye akaungana na Msigwa na mwalimu mwingine kumshambulia.
Alisema wakati akifanyiwa unyama huo, walimu wengine waajiriwa walikuwa kwenye ofisi nyingine wakifanya kikao, hivyo hawakujua kilichokuwa kikiendelea.
Alisema kuwa baadaye aliambiwa na Makamu Mkuu wa Shule hiyo aandike barua ya kuomba msamaha kwa kosa la kuwapiga walimu, jambo ambalo alidai hakukubaliana nalo lakini baada ya kutoa maelezo aliambiwa aandike barua ya kueleza tukio lilivyokuwa na ndicho alichokifanya.
Hivi sasa, mwanafunzi huyo anaendelea vizuri kiafya baada ya kupata matibabu kufuatia kuvimba baadhi ya maeneo mwilini na pia kuwa na jeraha karibu na jicho.

BABA ANENA
Baba wa mwanafunzi huyo, John Chinguku, ambaye ni mfanyakazi wa benki tawi la Mbozi, alinena mazito kwa kudai kuwa hadi sasa ni kama haamini kuwa mwanawe bado yuko hai kutokana na kipigo hicho cha walimu wake.
Akizungumza na Nipashe jana, Chingukwa alisema alistushwa mno baada ya kupata taarifa kupitia picha za video za ‘whatsapp’.
Hata hivyo, alisema ni jambo la kumshukuru Mungu kwamba mwanawe yuko hai kwa kuwa kipigo kilichokuwa kinaendelea kilihatarisha maisha yake.
Alisema ameridhishwa na hatua zilizochukuliwa na serikali hadi sasa na kusisitiza kuwa walimu wanapaswa kuzingatia weledi wa kazi zao na siyo kuadhibu watoto kwa namna ile aliyofanyiwa mwanawe.
 “Mimi nafanya kazi Mbozi na mama yao hawa vijana yupo Dar es Salaam, anamuuguza kaka yao ambaye anasumbuliwa na mguu, lakini pia pale nyumbani kwangu sina umeme ndiyo maana sikuweza kuwasiliana nao, lakini naishukuru Serikali kwa kuchukua hatua za haraka maana ile video inaonyesha wale walikuwa na makusudi mabaya,” alisema Chinguku.
Alisema baada ya kufuatilia fomu namba tatu (PF3) na kumchunguza kijana huyo ilibainika kuwa anaendelea vizuri.
MAWAZIRI WALIVYOINGILIA
Juzi, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia na Ufundi, Prof. Joyce Ndalichako, aliiambia Nipashe kuwa amelazimika kumvua madaraka mwalimu Mkuu wa shule hiyo pamoja na walimu ambao walifanya kitendo hicho baada ya kupata undani wa kilichotokea.
Prof. Ndalichako alisema baada ya kuona video ya walimu hao mtandaoni, aliwatuma Wadhibiti wa Ubora wa Shule Nyanda za Juu Kusini, Mbeya kulifuatilia na ndipo akachukua hatua hiyo.
Prof. Ndalichako alisema adhabu aliyopewa mwanafunzi huyo ni kinyume cha maadili ya kazi.
 “Nimeongea na mwalimu mkuu wa shule hiyo ananiambia alikuwa hajui tukio hilo, nilimuuliza kama yeye ni mkuu wa shule kweli, yaani tukio kama hili linatokea shuleni kwake hajui hadi analishuhudia kwenye mitandao ya kijamii,” alisema.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya nchi, Mwigulu Nchemba,alisema waliofanya tukio hilo watasakwa ili hatua zichukuliwe dhidi yao.
Waziri wa nchi ofisi ya Rais Serikali za Mitaa na Tawala za mikoa (Tamisemi), George Simbachawene, naye alitangaza kumshusha cheo Mwalimu Mkuu kwa kufumbia macho kitendo hicho na kutotoa taarifa mpaka video ilipozagaa mtandaoni.

Mwisho

Hakuna maoni