Breaking News

Wanasiasa wasemeeni wakulima pia


SHUGHULI kubwa ya kiuchumi kwa Watanzania walio wengi nchini, kimsingi ni kilimo.
Na kwa hali hiyo, si kupotoka nikisema kwamba walio wengi nchini ni wakulima.
Hii ni kwa sababu, kilimo ndiyo shughuli ya kiuchumi inayotegemewa na wananchi wengi wanaoishi vijijini.

Kwa mujibu wa takwimu za Sensa ya Mwaka 2012, asilimia 70 ya Watanzania milioni 45 wanaishi vijijini, huku asilimia 30 wakiishi mijini.
Kwa hali hiyo, serikali inaposisitizwa itoe kipaumbele kibajeti kwenye eneo la kilimo, ni kwa misingi kuwa, maendeleo yake yanagusa Watanzania wengi.
Kwamba serikali inapowekeza kwenye kilimo, inakuwa imewekeza kwa takribani asilimia 70 ya wananchi wake.
Mkulima 
Na uwekezaji kwenye eneo hilo unajulikana, kwa maana ya huduma anazozihitaji mkulima, kuwa ni pamoja na mbegu bora, zipatikane kwa bei nafuu na kwa wakati.
Mkulima anahitaji mbolea, awezeshwe kutoka kwenye jembe la mkono, aanze kutumia la kukokotwa na mifugo ama mashine kama matrekta.
Anahitaji dawa za kuua wadudu wamazao, ama kwa ajili ya palizi.
Anahitaji wataalamu wa kilimo ili azalishe kwa tija.
Anapovuna, aweze kupata soko la mazao yake, kama ni pamba, korosho, kahawa, mpunga, mahindi na mengineo.
Na kutokana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yameathiri hata uhakika wa mvua kwenye baadhi ya maeneo, mkulima anahitaji miundombinu ya umwagiliaji, ili aweze kuwa na uhakika wa maji kwa karibu kipindi chote cha mwaka.
Kimsingi uwekezaji wa kumwezesha mkulima apate huduma zote hizo, ndio unaotakiwa kwake.
Kwa bahati mbaya uwekezaji katika sekta hii umekuwa ukifanyika, lakini si kwa kiwango cha kuwawezesha wakulima wetu wafanikiwe.
Na ndiyo maana bado kuna kilio cha miaka mingi kutoka kwa kundi hili la wananchi, linalounda asilimia 70 ya Watanzania wote.
Kilio cha ukosefu wa mbegu bora, karibu katika maeneo yote ya nchi.
Kwa mfano katika kipindi cha miaka miwili iliyopita, kumekuwa na kilio cha wakulima wa zao la pamba kutoka kanda ya ziwa cha kuuziwa mbegu ‘feki’zilizosababisha wakakosa mavuno.
Na mbaya zaidi wanasiasa walitajwa kuwa nyuma ya kadhia hiyo, wakidaiwa kushiriki kuzipigia upatu, mbegu hizo kuwa ni mbegu bora.
Aidha kuna kilio cha wakulima wengi katika mikoa ya Rukwa, Ruvuma na hata ile ya Mtwara na Lindi, ya kucheleweshewa mbolea na dawa za kuua wadudu.
Lakini hata pale zilipofika kwa kuchelewa, bado bei yake ilikuwa ni ya ghali.
Aidha kuna kilio cha siku nyingi cha wakulima kukosa soko la uhakika la mazao yao, lakini pia mazao yao yakinunuliwa kwa bei ya chini isiyowawezesha kupiga hatua kubwa za kimaendeleo.
Kwa mfano katika mikoa ya Rukwa na Ruvuma, wakulima wanazalisha mahindi lakini si yote yananunuliwa.
Kwamba hata Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), anakosa bajeti ya kutosha kununua mahindi yote yanayozalishwa na wakulima.
Lakini pamoja na changamoto zote zinazoikumba sekta hii nchini, Muungwana anasikitishwa na kitendo cha moja ya wadau wa kundi hili, kutowasemea kama wanavyofanya kwa makundi mengine ya kijamii kama lile la wafanyabiashara.
Wadau ambao anawashangaa Muungwana kwa kukaa kwao kimya bila ya kusemea kwa mapana, changamoto hizi za wakulima kama wanavyofanya kwa kundi la wafanyabiashara ni wanasiasa, na hasa wale wa upinzani.
Ukiangalia kwa mfano kwenye sakata la mizigo bandarini na kwenye sekta ya utalii, lililotokana na hatua ya serikali kuanzisha Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), wanasiasa wa upinzani wamejitokeza kwa nguvu zote kulisemea.
Sasa sijui kwa sababu linawagusa wafanyabiashara!
Ni rai ya Muungwana kwa wanasiasa, na hasa wa upinzani, kuwa na kifua pia cha kuwasemea na wakulima pia.
Mwisho






Hakuna maoni